Jumanne, 11 Julai 2017

KIBWAGIZO CHA SIKUKUU
Kila mara tunadaiana aya za Biblia ili kuthibitisha hoja zetu. Jamani si lazima kila hoja ithibitishwe na aya fulani ya Biblia kwani sisi Wakatoliki tunaamini kwamba mafundisho yetu ya imani yanachimbuka kwenye Maandiko Matakatifu na Mapokeo Matakatifu. Mapokeo Matakatifu yapo katika mkufu wa kupokezana mafundisho mazuri toka enzi za Yesu hadi leo hii.
Tusisahau, walikuwepo watu walioishi, kula, kunywa na kuwagusa akina Yesu, Maria na kadhalika.Soma 1Yoh 1:1-4. Watu hao hawakuwa vipofu wala punguani. Tukubali macho, masikio na vichwa vyao vilirekodi mengi ya kweli. Kama wametuambia kitu tunaweza kuwasadiki. Hata Mtume Paulo alitumia Mapokeo Matakatifu kutangaza kweli za Kanisa. Soma 1Kor 11:23.
Ukisoma Yn 20:30-31 na 21:25 utaona kwamba kuna mengi ambayo hayakuandikwa kwenye Biblia. Sasa hayo yasiyoandikwa kwenye Biblia si kwamba yote ni uongo. Kumbe ili kuyapata yaliyo ya kweli kati ya hayo tunahitaji kutumia akili pia (Mt 22:37).
Hatumwabudu Mungu kwa mabavu na mtulinga tu. Tumeambiwa tutumie akili katika kumwamini Mungu. Kwetu sisi wakatoliki akili na imani havipingani. Ndiyo maana kuamini, kwa mfano, kwamba Pilato, Petro, Mtume Yuda Thadei, Mtume Yohane, Bartolomeo, Paulo, Barnaba, Maria Magdalena, Maria wa Kleopa na wengine wamekufa hatuhitaji kusoma katika Biblia habari za vifo vyao, la sivyo ingelitupasa kuamini kwamba wote hao bado wako hai kwa sababu Biblia inawaonesha wangali hai lakini hairipoti kwamba walikufa.
Na tena katika Biblia hiyo hiyo haijaandikwa kwamba ni lazima tuamini kilichoandikwa kwenye Biblia tu. Nionesheni aya ilipoandikwa kwamba inatupasa kuamini mambo yanayoandikwa kwenye Biblia tu. Mkionesha aya hiyo nitavua kofia yangu na kuibwaga mavumbini.HERI YA SIKUKUU KWENU NYOTE TENA!

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni